Thursday, August 11, 2011

Serikali kuajiri wahitimu 5,700 wa kilimo

SERIKALI inatarajia kuajiri wahitimu wa kilimo 5,770 wa kada mbalimbali katika mwaka huu wa fedha ulioanza Julai mosi ili kukabiliana na upungufu uliopo nchini.

Kwa mujibu wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, ajira za wahitimu hao zitatekelezwa na Serikali kupitia Wizara hiyo na ile ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi).

Halmashauri za wilaya, miji na manispaa zilizo chini ya tamisemi ndizo zitakazoajiri jumla ya wataalamu wa kilimo 8,500 ifikapo mwaka 2013.

Hayo yalisemwa jana na Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Rasilimaliwatu katika Idara ya Utawala na Maendeleo ya Rasilimaliwatu katika Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Mary Temba wakati akiwasilisha katika darasa la wakulima katika Maonesho ya Nanenane, kitaifa.

Temba aliwasilisha mada kuhusu Utaratibu wa ajira kwa wahitimu wa kada ya kilimo, kwenye maonesho hayo yanayofika kilele chake leo kwenye Viwanja vya Nzuguni mjini hapa.

Alisema ni azma ya Serikali kuhakikisha huduma za ushauri wa kilimo bora, umwagiliaji na ushirika zinawafikia wakulima /wafugaji katika kila kijiji, kata na tarafa kwa kuwa na wataalamu wa fani hizo karibu na wakulima.

Alisema katika wahitimu hao 5,770, walihitimu jumla ya wataalamu 4,550 katika ngazi ya Cheti na Diploma. Wahitimu katika ngazi ya Shahada katika fani ya kilimo walikuwa 785 na wa fani ya ushirika walikuwa 435.

“Wahitimu wote hawa wataajiriwa katika mwaka huu wa 2011/12 mara tu utaratibu wa kuwapanga utakapokamilika mapema Septemba baada ya kumalizika kwa vikao vya Bunge la Bajeti,” alisema Kaimu Mkurugenzi Msaidizi huyo.

Aliwataja waajiri watakaopangiwa kuwaajiri wahitimu hao kuwa ni Wizara yenyewe ya Kilimo, Chakula na Ushirika; Wizara nyingine za sekta ya kilimo, Halmashauri zote za wilaya, Jiji na manispaa pamoja na taasisi na bodi za mazao zilizo chini ya Wizara hiyo.

Alisema ni matarajio ya Wizara kwamba wahitimu wote wataitikia mwito wa Serikali wa kuwapatia nafasi hizo za ajira, na hivyo kila mmoja kuripoti pale atakapopangiwa na kutumia utaalamu wake kuwashauri vyema wakulima wa Tanzania kuhusu kilimo bora.

0 comments:

Post a Comment